Thursday, April 24, 2014

Hongera Serikali ya Tanzania, Mamlaka ya viwanja vya ndege (TAA) pamoja na Waziri Mwakyembe kwa kuanza ujenzi wa jengo kubwa la kisasa la uwanja wa ndege (TERMINAL 3)

Harakati za maandalizi ya ujenzi wa jengo jipya (Terminal 3) la uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), zimeanza rasmi. Hii ni habari njema kwa wadau wa sekta ya usafiri wa anga nchini. Kuanza kwa maandalizi ya ujenzi wa jengo hilo ni jambo lililokuwa likisubiriwa kwa hamu kubwa na wadau wa sekta ya usafiri wa anga ndani na nje ya Tanzania. Kukamilika kwa jengo hilo kubwa kutaleta mabadiliko makubwa sana katika huduma zitolewazo na pia kutaleta ufanisi wa hali ya juu katika huduma za usafiri wa anga na kuchangia kukuza uchumi wa Tanzania.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA), Ndugu Suleiman A. Suleiman amesema ujenzi wa jengo hilo ni miongoni mwa maboresho ya viwanja vya ndege nchini. Aidha Waziri wa Uchukuzi Mh. Harrison Mwakyembe amewahakikishia wananchi kuwa uwanja huo utakamilika kwa muda uliopangwa.

Blogu hii inaipongeza sana serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania kwa kuanza ujenzi wa jengo na uwanja (Terminal 3). Pia blogu hii inampongeza Waziri wa Uchukuzi Mh. Harrison Mwakyembe kwa kuwa chachu ya mafanikio ya ujenzi huu. Pia blogu hii imefurahishwa ba kauli ya Mh. Mwakyembe ya kuweka usafiri wa reli toka Airport kuelekea sehemu nyingine za jiji la Dar es Salaam. Blogu hii ina imani na serikali pamoja na Waziri husika kuwa ujenzi huu utakamilika kwa muda muafaka. Hii itatoa fursa kwa wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza katika jengo husika kama vile maduka ya kimataifa (Duty free shops). Maduka haya yatakuwa sawa na ya viwanja vingine vya kimataifa duniani. Pia kutakuwa na huduma nyingi kama vile restaurants na forex exchanges. Hakika uchumi wa Tanzania utakuwa kwa maana ya mashirika ya ndege ya kimataifa kuleta ndege zake kwa wingi na kuwafanya wawekezaji waliowekeza Tanzania kupata mapato makubwa kupitia vitu mbalimbali kama vile utalii, mahoteli n.k.

Blogu hii inapenda kutoa changamoto kwa serikali kuwa ni vyema ujenzi huu ukaenda pamoja na upanuzi wa barabara zetu hasa zile zitokazo Airport kuelekea katikati ya jiji la Dar es Salaam. Pia blogu hii inashauri kuwa ule usafiri wa reli toka uwanja wa ndege uwe wa kisasa na kwa viwango vya kimataifa kama vile ule usafiri wa reli toka uwanja wa Oliver Tambo International Airport jijini Johannesburg kuelekea PretoriaSouth Africa.



 
Picha toka: http://aviationtz.blogspot.com/

Tuesday, April 15, 2014

Hongera serikali ya Tanzania kwa kutoa na kuonyesha Hati ya Makubaliano ya Muungano ya mwaka 1964

Hongera serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa na kuonyesha Hati ya Makubaliano ya Muungano ya mwaka 1964. Kutolewa kwa hati hii muhimu kunaondoa hoja ya kuwa hakukuwa na Hati ya Makubaliano ya Muungano hapa nchini Tanzania.  Hati hiyo ilionyeshwa kwa waandishi wa habari kupitia Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue. Balozi Sefue alisema kuwa Rais Mh. Jakaya Kikwete ameridhia hati hiyo ionyeshwe hadharani. Hati hiyo imepigwa chapa na taipureta na ina takribani kurasa tatu huku jalada lake likiwa na rangi ya damu ya mzee. Aidha Hati ya Makubaliano ya Muungano ilisainiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Abeid Karume kwa wakati huo miaka takribani 50 iliyopita.

Blogu hii imefurahishwa na hatua hii njema ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuitoa hati hii muhimu kwa taifa letu. Pia blogu hii imefurahishwa na hatua ya Rais Mh Jakaya Kikwete ya kukubali kuitoa Hati hii hadharani. Ujasiri huu utaandikwa kwenye historia mpya ya Tanzania. Aidha blogu hii imefurahishwa kwa serikali kukubali kupeleka nakala zilizothibitishwa za Hati hii katika Makumbusho ya Taifa. Hii itatoa fursa kwa wananchi kuweza kuiona na kupunguza hoja kuwa Hati ya Makubaliano ya Muungano haipo.

Blogu hii inashauri serikali kuwa nakala za Hati hii ziwekwe pia kwenye Maktaba Kuu ya Taifa, pamoja na maktaba nyingine za mikoani pamoja na maktaba za vyuo vikuu nchini kikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) sehemu ya "East Africana". Hii itatoa fursa pana kwa wananchi, wasomi na watafiti kuweza kuiona. Kwa habari zaidi tembelea hapa.

Picha toka: Habari Leo (Gwiji la Habari Tanzania)
Balozi Ombeni Sefue, Katibu Mkuu Kiongozi akionyesha Hati ya Makubaliano ya Muungano jana jijini Dar es Salaam 

Thursday, April 10, 2014

Hongera JK kwa kuchaguliwa kuwa kiongozi mwenye mchango mkubwa zaidi katika maendeleo toka bara la Afrika mwaka 2013

Hongera Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Jakaya Kikwete kwa kuchaguliwa kuwa kiongozi mwenye mchango mkubwa zaidi katika maendeleo barani Afrika kwa mwaka 2013.

Rais Kikwete amepata tuzo hiyo kupitia jarida maarufu la kimataifa la `African Leadership Magazine Group'. Kwa kawaida tuzo hiyo hutolewa kwa kiongozi wa Afrika ambaye ametoa mchango mkubwa zaidi wa kijamii na kiuchumi. Kila mwaka tuzo ya aina hiyo hutolewa ambapo miaka ya nyuma walipata marais toka Liberia (Mh. Ellen Johnson Sirleaf) na Ghana (Mh. John Kuffor).

Rais kikwete ametunukiwa tuzo hiyo kwa kuendeleza utawala bora na kuifanya Tanzania kuwa nchi ya mfano kwa kuwa na mageuzi makubwa ya kisera na mifumo ya kiuchumi.

Blogu hii inapenda kuchukuwa nafasi hii kumpongeza Rais JK kwa kupata tuzo hiyo ya heshima. Heshima aliyopata Rais JK si ya kwake tu ila ni ya Tanzania kwa ujumla wake. Rais JK ameipata Tanzania heshima kubwa katika uso wa dunia hii. Aidha blogu hii inamwomba Mh Rais azidi kuimarisha utawala bora nchini na kufanya mageuzi ya kiuchumi na kijamii kwa maslahi ya watanzania wote. Pia blogu hii inawaomba viongozi walio chini ya Rais JK wafuate mfano wake ili Tanzania iweze kupiga hatua kubwa ya maendeleo. Sio nia ya blogu hii kutoa sifa lukuki ILA ukweli LAZIMA usemwe. Rais JK ndiye chachu ya kuleta amani na utulivu Zanzibar akishirikiana na viongozi wenzake. Chini ya Rais JK mwafaka ulipatikana Zanzibar. Pia chini ya Rais JK ameweza kutegua kitendawili cha kuandaa katiba mpya nchini Tanzania. Mambo hayo mawili SIYO madogo hata kidogo. Chini ya Rais JK barabara zimejengwa kwa kasi ya ajabu. Blogu hii kwa hakika kabisa inakubali kuwa bado kuna changamoto za kimaendeleo nchini Tanzania LAKINI kwa kiasi kikubwa Rais JK amejitahidi sana. 

Mwisho blogu hii inapenda kumwomba Rais azidi kuwaletea wananchi wa Tanzania maendeleo licha ya changamoto za hapa na pale. Mwenye macho aambiwi TAZAMA. Kwa habari zaidi soma dailynews na nipashe.

Picha: e.wikipedia.org

Tuesday, April 8, 2014

Hongera Timu ya watoto wa mitaani ya Tanzania kwa kutwaa kombe la dunia la mpira wa miguu nchini Brazil

Hongera Timu ya watoto wa mitaani ya Tanzania kwa kutwaa kombe la dunia la mpira wa miguu nchini Brazil jana. Timu ya watoto wa mitaani ya Tanzania iliwafunga watoto wenzao toka nchini Burundi kwa jumla ya mabao 3 kwa 1 katika fainali zilizofanyika nchini Brazil. Blogu hii inawapongeza vijana hawa pamoja na walimu wao kwa kuliletea heshima taifa la Tanzania. Vile vile blogu hii inapenda kuwapongeza waandaaji wa watoto hawa yaani Tanzania Street Children Sports Academy (TSCSA) kwa maandalizi mazuri waliyofanya na kufanikisha kombe la dunia kuja Tanzania. Hakika TSCSA imejenga heshima kwa watanzania kwa kuwa taasisi makini katika maendeleo ya mchezo wa kandanda nchini kupitia watoto wa mitaani.

Hakika vijana wa mitaani  wa Tanzania wamepeperusha vyema bendera ya Tanzania. Ni matarajio ya blogu hii kuwa watoto hawa warudipo Tanzania wataendelezwa na kuingizwa kwenye programu kupitia "academy" ambazo wadau wa michezo nchini wanazo ama wanapaswa kuwa nazo.

Siku zote maendeleo ya mpira ama mchezo wowote huanzia chini na hasa mitaani. Hivyo ni jukumu la wadau wa kandanda kama chama cha mpira wa miguu nchini (TFF), Wizara inayohusika na Michezo na ile ya Elimu kuendeleza vipaji hivi. Blogu hii inakumbusha pia kuwe na ligi fupi za watoto na vijana kwa kila kanda nchini na wakati huo huo kuwe na michezo ya shule za msingi, sekondari na vyuo kikanda na kitaifa ili kuweza kuibua vijana wenye uwezo ili wazidi kuliletea taifa letu heshima duniani.


Picha: bongostaz