Friday, December 27, 2013

Waziri wa Elimu Dr Kawambwa amewaagiza Maafisa Elimu nchini kuhakikisha walimu wapya wanalipwa stahili zao mapema

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dr Shukuru Kawambwa amewaagiza Maafisa Elimu wa mikoa na wilaya nchini kuhakikisha walimu wapya wanalipwa stahili zao mapema. Aidha waziri huyo amewaagiza maafisa hao wa elimu kuhakikisha walimu wapya wanapokelewa vizuri katika maeneo yao ya kazi.


Blogu hii inapenda kumpongeza Waziri Dr Kawambwa kwa kauli hiyo ya kuwataka maafisa elimu nchini kuhakikisha walimu wapya wengi wao wakiwa walimu vijana kulipwa stahili zao mapema. Hii itawafanya walimu hao wapya wasikatishwe tamaa ya kukaa katika vituo vyao walipopangiwa. Pia kuwajali walimu hasa wanapoajiriwa kwa mara ya kwanza inakuwa kama motisha kwao. Aidha Waziri amewaagiza maafisa hao kuhakikisha kuwa wanafuatilia suala zima la ufundishaji mashuleni na kuwa na walimu wakuu wenye sifa. 


Aidha blogu hii inaomba, wizara ya elimu kwa kushirikiana na TAMISEMI kufuatilia kwa karibu ili kuhakikisha walimu hao wapya wanapokelewa vizuri na wanahudumiwa ipasavyo. Ni vyema kukawa na ufuatiliaji wa karibu katika kuhakikisha walimu wanapatiwa mahitaji yao ya lazima na hasa kwa hawa wlimu wapya.


Duniani kote mwalimu ni nguzo ya Taifa na hakuna maendeleo bila elimu bora na elimu bora inatoka kwa mwalimu aliyeandaliwa na kuhudumiwa vizuri. Kwa habari zaidi soma majira


Picha: 24tanzania

Monday, December 16, 2013

Hongera Rais JK kwa kutoa hotuba nzuri sana katika mazishi ya MANDELA kijijini kwake Qunu

Sikiliza hotuba ya JK Qunu katika mazishi ya MANDELA 15/12/2013

Picha:Pool/AFP, Odd Andersen


Jana tarehe 15/12/2013 nikiwa nyumbani kwangu nikiangalia matangazo ya moja kwa moja ya luninga toka Qunu nchini Afrika ya Kusini kupitia chaneli ya MADIBA niliona na kusikiliza mambo mengi lakini mojawapo ni hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh Jakaya Mrisho Kikwete. Hakika katika hotuba hiyo JK alifunika. Kikwete aliwakumbusha wananchi wa Afrika ya Kusini walipotoka katika masuala ya kukomboa nchi yao. Kikwete aliwakumbusha wasauzi kuwa Tanzania iliwapa hifadhi pamoja na baadhi yao hati za kusafiria. Mandela alipewa yote hayo! Wasauzi enzi za ubaguzi wa rangi iliwapa hifadhi katika maeneo kama vile Kongwa, Mgagao, Mazimbu, Dakawa nk. 

Rais JK alisema Tanzania ilitoa ushirikiano wa hali ya juu na kusimamisha maendeleo yake kwa ajii ya Afrika ya Kusini. Wakati Mandela alipokuja Tanzania hakuwa na hati ya kusafiria "passport" ila alipewa "travel documents" toka Tanzania na aliweza kusafiri nchi mbalimbali. Tanzania ilianzisha Radio Freedom iliyokuwa inatangaza toka Tanzania Dar es Salaam kwa ajili ya ukombozi wa wananchi waliokuwa wanabaguliwa wa Afrika ya Kusini. Radio hii ilisaidia kuimarisha juhudi za ukombozi kusini mwa Afrika. Pia JK alisema, MANDELA alipokuwa anakuja Tanzania alikuwa haishi hotelini bali kwa watu binafsi ili kulinda usalama wake.

Hakika JK amewafungua macho na masikio wasauzi juu ya uhusiano uliokuwepo kati ya wananchi wa nchi hizi mbili na hasa wakati wa ukombozi. Hakusau kusema kuwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipigania sana ukombozi wa wananchi wa Afrika ya Kusini na alikuwa rafiki wa MANDELA. MANDELA alianza kutembelea Tanzania kutoka Afrika ya Kusini akipitia Northern Rhodesia, Tanganyika (Town of Mbeya) mpaka Dar es Salaam kwa ajili ya kuomba msaada wa ukombozi na kupatiwa mafunzo ya wapigania uhuru na ubaguzi wa rangi.

JK alisema, Mandela alipotolewa gerezani na kutembela Tanzania miaka ya 90 alipokelewa na wananchi wengi waliokuwa na shauku ya kumuona mwanamapinduzi huyo. JK alisema licha ya mvua kubwa wananchi wa Tanzania walizidi kujitokeza kumshangilia. Nakumbuka wakati huo na mimi nilipata fursa ya kumuona akiwa pamoja na Mwalimu Nyerere na Winnie Mandela kwenye gari la wazi wakielekea Ikulu toka uwanja wa ndege wa Dar es Salaam.

Blogu hii inampongeza sana JK kwa kutoa hotuba nzuri na kuwaeleza jinsi Tanzania ilivyoshiriki kikamilifu katika ukombozi kusini mwa afrika na hasa ukombozi dhidi ya ubaguzi wa rangi.

Blogu hii inaomba taasisi husika ziweze kutunza kwa umakini na umaridadi mambo yote ili vizazi vijavyo na wageni waweze kujua jinsi Tanzania ilivyoshiriki katika ukombozi. Maeneo yote ambayo kulikuwa na historia ya ukombozi hasa maeneo ya Morogoro yawe chini ya makumbusho ya Taifa ili pamoja na mambo mengine iwe mojawapo ya pato la taifa kupitia wageni toka nje nchi. Pia kuwe na matangazo kupitia radio, luninga, magazeti, internet juu ya historia, makumbusho na vitu vya kale vilivyopo Tanzania. Wenzetu mambo haya yanaingiza fedha na sisi tuchangamke!

Sikiliza hotuba ya JK Qunu katika mazishi ya MANDELA 15/12/2013

Sunday, December 8, 2013

Hongera sana IVO MAPUNDA kwa kutupeleka NUSU FAINALI kombe la Challenge nchini Kenya

HONGERA kipa wa KILIMANJARO stars IVO MAPUNDA. Katika mechi ya robo fainali ya kombe la challenge dhidi ya Timu ya Taifa ya Uganda, mlinda mlango huyo ambaye kwa sasa yupo nchini Kenya akidakia moja ya vilabu nchini humo ameonyesha umahili wa hali ya juu sana. Katika mechi hiyo ya robo fainali iliyofanyika jumamosi tarehe 7 disemba 2013, MAPUNDA aliokoa penati mbili ambazo ziliiwezesha Kilimanjaro stars kutinga Nusu Fainali. MAPUNDA alikuwa kipa namba moja wa Timu ya Taifa ya Tanzania miaka ya nyuma lakini baadae alitemwa!! Mwaka huu kocha wa Timu ya Taifa ya Bara alimjumuisha kwenye kikosi cha Kili stars.

Lakini MAPUNDA inaonekana sasa amerudi kwenye kiwango chake na ameonyesha uwezo na kujituma. Hakika blogu hii inampongeza MAPUNDA kwa kutupeleka NUSU FAINALI lakini pia kwa kulipigania TAIFA kwa umahili mkubwa. Kwa walioangalia mechi ile na zingine watakubaliana na blogu hii kuwa MAPUNDA alijituma sana na kuonyesha juhudi kubwa. Blogu hii inaomba wachezaji wengine wa kitanzania waonyeshe juhudi kama alivyoonyesha MAPUNDA. Kwa kucheza kwa juhudi kama alivyofanya MAPUNDA kunaweza kutufikisha mbali katika mashindano ya kimataifa.

Picha:footballzz.com

Tuige siasa za Komredi MANDELA kumuenzi _ aliwaunganisha watu wote bila ya kubeza wengine!

Hakika Kifo cha Komredi Nelson Mandela wenyewe wanamwita MADIBA kimetikisa dunia hasa Tanzania. Kiongozi huyu tunaweza kusema ni wa kufikirika! Alipinga ubaguzi wa rangi dhidi ya utawala wa makaburu kule Afrika ya Kusini. Alifungwa zaidi ya miaka 27 na kuteswa sana. Licha ya mateso hayo alizidi kuwa mtetezi wa wanyonge akiwa gerezani na kukataa msamaha wenye masharti.

Baada ya kutolewa gerezani miaka ya tisini alichaguliwa kuwa Rais wa kwanza mweusi katika utawala wa kidemokrasia nchini Afrika ya Kusini. Kikubwa ambacho wengi KINATUSHINDA! ni kuwa aliwasamehe wote waliomkosea wakati wa UBAGUZI WA RANGI!! Aliwasihi waafrika weusi WASILIPIZE KISASI dhidi ya wazungu! Aliwahimiza WAAFRIKA weusi wasiwabeze na kuwasimanga WAZUNGU ila washirikiane kujenga TAIFA JIPYA. 

Mandela aliamini adui alikuwa ni ubaguzi wa RANGI!!! na sio RANGI ya MTU!! Kibinadamu sio rahisi kusamehe watu waliokupa mateso makali. Mandela aliepusha mauaji ya kisasi dhidi ya wazungu. Kama angekuwa kiongozi wa visasi, Afrika Kusini kungekuwa na mauaji ya kutisha dhidi ya watu weupe. Hii ingetokana na waafrika weusi kulipiza kisasi na kuwabeza weupe!! Mandela alikataa hayo yote na kuchukuliwa wananchi wote wa Afrika ya Kusini kama kitu kimoja bila kujali RANGI ya MTU!! Hakika Dunia itamkumbuka sana Mandela!

Blogu hii inaomba hulka, tabia na mwenendo wa MANDELA uigwe na VIONGOZI wa sasa ndani ya DUNIA hii ambayo tupo kwa MUDA tu. Blogu hii inaomba siasa za kubezana, za visasi na zisizo na tija kuepukwa na viongozi na watu wote. Lengo kwa wote ni kuleta maendeleo na sio kubezana na siasa zisizo msaidia mtu wa kawaida. Ukiangalia MANDELA hakuwahi hata siku moja kufurahia udhaifu wa wengine mara baada ya kuwa RAIS wa Afrika Kusini ila aliwashika mkono hata wale walioaminika kuwa walikuwa maadui zake enzi za ubaguzi wa RANGI.

Hakika, MANDELA ni SOMO kubwa kwa WAAFRIKA, katika kuleta ustawi na maendeleo ya kistaarabu ya bara hili lenye migogoro isiyo na tija.

R.I.P MANDELA!! MWENYEZI MUNGU UIWEKE ROHO YAKE MAHALA PEMA PEPONI AMINA!!!
Picha:consortiumnews.com