Tuesday, December 23, 2014

Asante Rais KIKWETE kwa kuwabeba watanzania kupitia hotuba ya kuhitimisha sakata la Tegeta ESCROW

Picha: tanzaniatoday.co.tz

Jumatatu, ya tarehe 22 Desemba 2014 itakuwa siku ya kukumbukwa na watanzania ambapo Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mh Dr. Jakaya Mrisho Kikwete alipohutubia taifa kupitia wazee wa jiji la Dar es Salaam. Kwa namna ya pekee kabisa blogu hii inampongeza kwa dhati Rais kwa hotuba yake nzuri katika kuhitimisha sakata la “account” ya Tegeta ESCROW.  

Rais alielezea historia nzima kiasi kwamba watanzania wengi wamepata uelewa mpana wa suala lenyewe. Aidha kwa namna ya pekee blogu hii inamshukuru kwa dhati kabisa kwa kukubaliana na mapendekezo ya Bunge letu tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kitendo cha Rais kuwashukuru wabunge wote ni cha kuigwa na watanzania wote.

Blogu hii haina haja ya kueleza hatua gani zimechukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa juu ya suala hili lakini hatua ya Rais ya kulivalia njuga suala hili kupitia hotuba yake kumeleta mwanga wa matumaini kwa watanzania na kuongeza utulivu na amani nchini. Kwa hakika blogu hii imeona ni kwa jinsi gani watanzania wasivyopenda vitendo viovu viendelee kutamalaki katika jamii zetu. Blogu hii imeshuhudia pia hata wapenzi wa chama tawala wamefurahishwa na hatua ambazo Rais amechukuwa za kupambana na maovu kupitia sakata hili. 

Kwa namna ya pekee blogu hii imefurahishwa kwa namna ambavyo Rais alivyo/anavyo chukua hatua juu ya sakata hili bila kuleta migongano kwa mihimili mingine na kwa jinsi anavyochukuwa tahadhari kuhakikisha haki inatendeka kwa kufuata sheria na taratibu za nchi. Kufuata haki, sheria na taratibu za nchi hata kwa wanaotuhumiwa katika sakata hili ni jambo zuri na linafaa kuigwa kwa viongozi wengine ndani na nje ya nchi yetu ili kuondoa dhana ya kumwonea mtu. Hii inadhihirisha utawala wa haki, sheria na kidemokrasia.

Blogu hii inaomba suala la maadili kwa wote na hasa watumishi wa serikali na viongozi wa umma litiliwe mkazo unaostahili. Tume ya Maadili ipewe nguvu zaidi, ipewe rasilimali watu zaidi na vitendea kazi bora ili iweze kufuatilia masuala ya kimaadili kwa ustadi mkubwa. Aidha mapambano ya rushwa yanatakiwa kupewa nguvu zaidi kwa kuimarisha taasisi ya kupambana na rushwa katika ngazi zote ikiwemo hata kwa serikali za mitaa ambapo ndipo chimbuko la uongozi wa nchi. 

Mwisho viongozi wapewe mafunzo ya uongozi, wajue uongozi ni dhamana, wajue wananchi ni nani na nini matarajiyo yao kutoka kwao. Miaka iliyopita chuo cha Kivukoni kilitumika pamoja na mambo mengine kuwaandaa na kuwapa maadili viongozi. Blogu hii inaomba utamaduni na utaratibu huo urudi, ili viongozi na hasa viongozi vijana wajue nini maana ya uongozi. Hii italifanya taifa letu lipige hatua kubwa ya maendeleo.


Asante JK kwa kuwabeba watanzania.   

Sunday, December 14, 2014

WANAWAKE WANAWEZA!!!! Hongera Jonisia Rukyaa kwa kuwa mwanamke wa kwanza kuchezesha MECHI kubwa ya SIMBA na YANGA ya NANI MTANI JEMBE 2

Hongera mwanamama (Jonisia Rukyaa) toka mkoa wa Kagera kwa kuwa mwanamke wa kwanza nchini Tanzania kuchezesha mechi kubwa ya watani wa jadi, Simba Sports Club (Simba) na Young Africans Sports Club (Yanga) kupitia shindano la Bia ya Kilimanjaro ya NANI MTANI JEMBE 2. Katika mechi hiyo iliyofanyika jana (jumamosi, 13/12/2014) jijini Dar es Salaam katika uwanja wa Taifa, ambapo SIMBA waliibuka na ushindi wa mabao 2 kwa 0. Blogu hii inaomba wanawake wengine wajitokeze katika nyanja mbalimbali hususan michezo ili kufuata nyayo za mwanamama huyu hodari.

Hakika blogu hii inakupongeza sana licha ya changamoto chache zilizojitokeza ambazo hata upande wa waliopoteza (YANGA) wanazikubali. Blogu hii inakuomba utafute mkanda wa mechi ile na uondoe makosa machache ambayo WOTE tuliyaona. Ila kwa kiasi kikubwa ulijitahidi sana. Big UP mwanamama, Kweli WANAWAKE wanaweza!! Tembelea michuzi ujionee picha za mchezo huo muhimu.

Picha: Michuzi blog

Wednesday, December 10, 2014

Hongera Idris Sultan kwa kujizolea kitika, takriban milioni 500 za kitanzania toka shindano la Big Brother Hotshots nchini Afrika Kusini

Hongera Idris Sultan kwa kujizolea kitika, takriban milioni 500 za kitanzania. Blogu hii imefurahishwa na ushindi huu ulioupata toka BBA katika shindano la Big Brother Hotshots nchini Afrika Kusini. Ushindi huu si wa Idris pekee bali ni ushindi wa watanzania wote. Ushindi huu pia unawafundisha vijana wengine wa kitanzania katika nyanja zote za michezo, sanaa na muziki kuwa inawezekana kupata ushindi. Blogu hii inaomba vijana wengine katika nyanja zote waige mfano wa kujituma bila ya kukata tamaa kama alivyoonyesha Idris katika shindano hili. Hongera sana Idris. Kwa habari zaidi bofya

Picha:bigbrotherafrica


Monday, December 1, 2014

Hongera Bodi ya Utalii kwa kutangaza vivutio vya utalii vyaTanzania kupitia Ligi Kuu ya Uingereza

Picha:tanzaniatoday.co.tz

Hongera Bodi ya Utalii ya Tanzania kwa kutangaza vivutio vya utalii kupitia ligi maarufu duniani, Ligi Kuu ya Uingereza. Kila mmoja wetu anajua umaarufu wa Ligi hii duniani. Ni ligi inayofuatiliwa na kutazamwa na watu wengi sana duniani kupitia njia mbalimbali ikiwemo matangazo ya Luninga. Katika mechi kati ya Sunderland na Chelsea ambapo wachezaji wa Sunderland walivalia jezi za mazoezi (T-shirts) zilizokuwa na tangazo “Visit Tanzania” Mechi hiyo iliyofanyika nchini Uingereza iliishia kwa timu hizo kutoka suluhu ya bila kufungana. Ni matumaini ya blogu hii watu wengi walitazama tangazo hilo na hata kumbukumbu kubaki katika mitandao mbalimbali duniani. 

Hakika hili ni jambo zuri kwa maana lina mchango mkubwa katika kuinua uchumi wa taifa kupitia utalii. Tanzania ni nchi yenye vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mbuga ya Serengeti, Mikumi, Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro, vivutio vya Zanzibar na Bagamoyo nk. Kupitia Tangazo hili nchi yetu itatembelewa na watalii wengi zaidi na kuchangia pato la mtu mmoja mmoja na taifa kwa jumla.

Blogu inaipongeza serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania kupitia kwa Rais Jakaya Kikwete kwa kuitangaza Tanzania. Vile vile Bodi ya Utalii pamoja na Wizara husika zinastahili pongezi za dhati. Juhudi hizi zinapaswa kuendelezwa. Blogu hii inaishauri serikali kwa kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kuongezeka kwa abiria (watalii) kupitia viwanja vyetu vya ndege, hivyo ni wakati muafaka wa kiviboresha zaidi na kuwa na hadhi na mahitaji ya kimataifa. Blogu hii inatambua upanuzi wa kiwanja cha Mwalimu Julius Nyerere cha Dar es Salaam, hata hivyo viwanja vingine hasa Kilimanjaro, Mwanza na Zanzibar vinapaswa kuboreshwa ili kupokea wingi wa watalii na wageni toka nje ya nchi.

Kwa habari zaidi tembelea Tanzania tourist board  uone vivutio vilivyoko Tanzania.

Sunday, November 30, 2014

Pole na karibu Rais Mh Jakaya Mrisho Kikwete toka nchini Marekani

jk3
Picha:dewjiblog.com

Blogu hii inapenda kukupa pole Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Jakaya Mrisho Kikwete kwa kurudi salama Tanzania toka Marekani ulipokuwa unashughulikia afya yako. Afya yako ni afya ya watanzania wote. Blogu hii imeona ni busara kukupa pole kwa niaba ya watanzania na kukukaribisha tena ili kuzidi kuwaletea maendeleo wananchi.


Blogu hii imefurahishwa na ujasiri wa kuelezea afya yako kwa wananchi siku ya Jumamosi tarehe 29 mwaka 2014 ulipowasili toka nchini Marekani. Hakika umetufundisha somo la kupima afya zetu mara kwa mara ili kubaini tatizo mapema. Somo hili hasa la kupima afya mara kwa mara ni muhimu ukizingatia watanzania kutokuwa na utamaduni huo hata kama kuna fursa ya huduma za afya.  Pole sana Rais wetu na karibu nchini uzidi kuwaletea wananchi maendeleo.

Hongera Mh Mizengo Pinda kwa busara, subira na uvumilivu wakati wa mjadala wa sakata la Tegeta ESCROW ndani ya Bunge

Image result for pinda mizengo
Kwa namna ya pekee blogu hii inampongeza Waziri Mkuu “mtoto wa mkulima” Mh. Mizengo Pinda kwa busara, heshima, ustahimilifu na subira juu ya Sakata la “account” ya Tegeta ESCROW. Hakika umetufundisha kitu katika sakata hili na kudhihilisha kuwa uongozi ni kujali maslahi mapana ya wananchi na siyo vinginevyo. 

Blogu hii inakupongeza kwa jinsi ulivyotoa maneno ya kuwaunganisha watanzania wakati wa kufunga Bunge jumamosi tarehe 29 mwaka 2014. Ustahimilifu, subira, heshima, busara uliyoonyesha ni SIFA ya KIONGOZI MKUU. Hakika SIFA hizo unazo. Pia blogu hii imependa kauli zako ikiwemo “Yaliyopita si ndwele tungange na yajayo”, ni kauli nzuri kwa ustawi wa taifa lolote.

Ni matumaini ya blogu hii na watanzania kuwa mapendekezo ya wabunge wetu wote juu ya sakata hili yatafanyiwa kazi kwa uadilifu na uaminifu mkubwa chini ya UONGOZI WAKO. Blogu hii imejionea kuwa kauli zako katika suala hili ni za kuwaunganisha watanzania. Aidha ahadi ulizotoa zimewafuta machozi watanzania wote bila kujali itikadi zao.

Hongera wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kusimamia sakata la Tegeta ESCROW

Picha: thehabari.com

Hongera wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi mlivyosimamia suala zito la Sakata la “account” ya Tegeta ESCROW. Blogu hii inaamini suala hili lilikuwa nyeti, gumu na lililokuwa linagusa nyoyo za watanzania. Ni suala ambalo lilikuwa na majibu mawili moja kujenga ama kubomoa taifa. Hakika wabunge wote mmerudisha imani kwa wananchi wa nchi hii kwa kuweka mbele maslahi mapana ya nchi yetu. Wabunge mmetukumbusha kuwa uongozi ni dhamana, uongozi ni uadilifu, uongozi ni uwajibikaji, uongozi ni ukweli. Kiongozi asiye mkweli ni tatizo, kiongozi asiye mwadilifu ni tatizo. 

Blogu hii inaomba kuwataja wabunge wachache kwa niaba ya wabunge wote kwa jinsi walivyosaidia kuwatetea na kuwaunganisha watanzania, Mh Zitto Zuberi Kabwe, Mh Deo Filikunjombe, Mh Mwigulu Nchemba, Mh David Kafulila, Mh James Mbatia, Mh Ole Sendeka, Mh Dr Hamisi Kingwangala, Mh William Lukuvi, Mh Freeman Mbowe, Mh Kangi Lugola, Mh Stephen Wasira, Mh John Mnyika nk.  

Blogu hii inaomba mwelekeo huu uendelee hata katika masuala mengine ya kitaifa, na bila kusahau wajibu wenu wa kuwawakilisha wananchi na kuisimamia serikali ili ilete maendeleo ya kweli kwa wananchi wake. Hakika siku ya Jumamosi tarehe 29 mwaka 2014 ni siku ya kukumbukwa kwa taifa letu. Mwenyezi MUNGU awabariki WABUNGE wote wa BUNGE hili kwa kutenda HAKI na KUWABEBA WATANZANIA.

Hongera kamati ya PAC chini ya Mh Zitto na Mh Filikunjombe juu ya sakata la Tegeta ESCROW

Image result for zitto kabweImage result for filikunjombe
Hongera Mh. Zitto Kabwe na Mh. Deo Filikunjombe pamoja na wajumbe wote wa kamati ya “PAC”. Hakika mmewatendea haki watanzania katika kipindi chote cha uchunguzi, uchambuzi na uwasilishwaji wa maadhimio yaliyohitimishwa Jumamosi tarehe 29 mwaka 2014. 

Sakata la “account” ya Tegeta ESCROW halikuwa jambo dogo. Uimara na umahili wenu kwa kusaidiana na wajumbe wote wa PAC umewafuta machozi watanzania bila kujali itikadi ya vyama. Kamati yenu, imetukumbusha kuwa “cheo ni dhamana”, imetukumbusha “cheo siyo dharau”, imetukumbusha “uongozi ni uadilifu, ukweli, kutenda haki na uaminifu.  

Kazi yenu imeleta heshima ya nchi yetu, na kurudisha imani kwa watanzania kupitia wawakilishi wao. Aidha mmesaidia kuokoa rasilimali za nchi hii kwa wakati huu na kwa miaka ijayo, mmedumisha nidhamu kwa wote hususan watendaji na viongozi. 

Blogu hii inawapongeza sana, Mwenyezi Mungu Awabariki Sana. Blogu hii inapendekeza nchi yetu itilie mkazo suala la MAADILI siyo kwa viongozi wa umma pekee ila hata kwa watendaji wote ikiwemo sekta binafsi. 

Kuwepo na vyombo vya kuhakikisha nidhamu inakuwepo kwa watu wote. Blogu hii inafurahi uwepo wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa “PCCB”, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali “CAG”, Ofisi ya Maadili nk. Blogu hii inaomba vyombo hivi vipewe nguvu na nyenzo zaidi kikatiba ili kulinda maslahi ya Taifa letu. Kazi ya kwanza kwa vyombo hivi na vingine ikiwemo Polisi, Usalama wa Taifa ni kulinda maslahi ya nchi yetu ikiwemo ya kiuchumi pamoja na rasilimali za nchi. 

Kuna haja ya vyombo hivi na vingine vikafanya kazi kwa ushirikiano ili kuleta ufanisi wa kimaadili, usalama na uzalendo. Suala la usalama ni pamoja na ulinzi wa rasilimali za Taifa ikiwemo pesa za serikali na walipa kodi. 

Hongera Mh. Mama Anne Semamba Makinda kwa KUWABEBA WATANZANIA kwa kusimamia sakata la Tegeta ESCROW

Image result for anna makinda
Hongera Mh. Mama Anne Semamba Makinda kwa uongozi uliotukuka katika kusimamia sakata la Tegeta ESCROW. Haikuwa kazi nyepesi hata kidogo! Ubunifu wako wa maridhiano, subira, heshima kwa wote, watanzania wameiona. Mama Makinda, blogu hii ya “tuijengetanzania” inatoa pongezi za dhati kwa jinsi ulivyosimamia na kuendesha Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania, hususan katika sakata hili na kuweza kuhitimisha maadhimio ya Bunge zima siku muhimu ya Jumamosi tarehe 29 mwaka 2014. 

Kukubali kwako kuiamini na kuipa kazi kamati ya “PAC” chini ya Mh. Zitto Kabwe na Mh. Deo Filikunjombe kumeleta matumaini mapya kwa watanzania. Pia uongozi wako uliotukuka umewatendea haki watanzania wote. Hakika umetufundisha kazi ya Bunge ni kuisimamia na kuishauri serikali na siyo vinginevyo. Umetukumbusha kazi ya wabunge ni ya wananchi na pia umetukumbusha wananchi wanawategemea wabunge wao ambao ni wawakilishi wao. 

Pia umetukumbusha msemo wakati wa Mwalimu Nyerere usemao “Nitasema kweli daima, fitina kwangu mwisho”. Kazi uliyoifanya siyo imeongeza sifa ya Bunge letu tukufu bali pia imelinda rasilimali za nchi hii sasa na siku za usoni. Umetukumbusha MAADILI kuwa ni jambo muhimu katika kuwaletea maendeleo wananchi. Blogu hii inakuomba kupitia Bunge lako Tukufu kuhakikisha suala la MAADILI kwa wote (viongozi, watendaji na wananchi) linatiliwa mkazo na kunakuwa na vyombo vya kulazimisha watu wafuate maadili mema. Vyombo kama polisi, usalama wa taifa, CAG, PCCP na vinginevyo kufanya kazi na kuwapeleka wahusika pasipo kusubiri Bunge kujadili tuhuma. Kwa maneno mengine tuhuma hizi zinatakiwa kumalizwa na vyombo hivi na nchi kuwa salama.

Suala la maadili ni pana na si kwa viongozi pekee, ni suala hata mitaani watu wanapaswa kuwa waadilifu katika mambo mengi sana mfano kuna tabia ya watu wadogo mitaani kutukana matusi bila kuogopa wala kuchukuliwa hatua yoyote, kuna vitendo vya unyanyasaji wa watoto wadogo toka kwa ama wazazi, walezi ama watu wazima, kuna rushwa ndogo ndogo, kuna watendaji wa chini kutotimiza wajibu wao mfano mzuri uwepo wa uchafu katika mitaa tunayoishi, hapa ni kuwa kuna ukosefu wa maadili hata kwa watu wa chini.

Pia suala la MAADILI lipelekwe kwenye shule zetu tokea chekechea mpaka Vyuo Vikuu. Watoto wafundishwe haki, usawa, utu, kukataa rushwa nk tangia wakiwa wadogo. Mitaala yetu pamoja na mambo mengine ijikite katika maadili. Sifa ya kiongozi na mwananchi iwe UADILIFU. 

Kuna wakati mdau wa blogu hii aliwahi kutembelea nchini Sweden, huko alikutana na jambo dogo lakini kubwa kimaadili, kuna mtoto wa shule moja ya msingi alichukuwa kalamu ya rafiki yake shuleni kwa bahati mbaya, alipofika nyumbani na kubaini amechukua kalamu ya mwenziye, alimshauri baba yake ampeleke nyumbani kwa rafiki yake ili amrudishie kalamu yake, baba yule akasema utampa kesho, mtoto yule hakufurahi! Nini maana yake? Ni kuwa suala la MAADILI linaanzia shuleni, linaanzia tokea utoto, linajengwa tangu awali.

Blogu hii inaamini kuwa maendeleo ya kweli yatakuja kwa kila mmoja kuwa na maadili mema apende asipende. Hakika blogu hii inakutakia maisha marefu katika utumishi wako uliotukuka. Hakika nani kama Mama, hakuna. Asante Mama Anne Semamba Makinda kwa KUWABEBA WATANZANIA, MWENYEZI MUNGU AKUBARIKI HAPA DUNIANI NA HATA MILELE AMINA


Monday, November 17, 2014

Hongera Wizara ya Ujenzi kwa kuleta kivuko kitakachotoa huduma kati ya Bagamoyo hadi Dar es Salaam

Hongera Wizara ya Ujenzi, hususan waziri wake Mchapakazi Mh Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutimiza ahadi na kuleta kivuko kitakachotoa huduma ya usafiri kati ya Bagamoyo hadi katikati ya jiji la Dar es Salaam kupitia mwambao wa bahari ya hindi. Pongezi za jumla ziende kwa serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mh. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kutimiza ahadi ya kufanikisha ujio wa kivuko hiki muhimu. Aidha, blogu hii inaipongeza TEMESA "Wakala wa Ufundi na Umeme" kwa kufanikisha jambo hili muhimu kwa wananchi wakazi wa Dar es Salaam na Bagamoyo. 

Huduma ya kivuko (Mv Dar es Salaam) hiki kitapunguza adha ya usafiri kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam, hususan wale watokao Bagamoyo kupitia mwambao wa Bahari ya Hindi hadi katikati ya jiji. Kivuko hiki kitawasaidia wakazi wa Bagamoyo, Bunju, Tegeta, Boko, Kunduchi nk kuwahi kufika katikati ya jiji la Dar es Salaam na kuokoa muda mwingi unaopotea.

Kivuko hiki ni muendelezo wa juhudi za Wizara ya Ujenzi kupitia kwa Mh. Magufuli katika kupunguza msongamano ndani ya jiji la Dar es Salaam kama vile ujenzi wa barabara ya New Bagamoyo toka kwenye makutano ya barabara ya Kawawa kwenda Tegeta, miundombinu ya mabasi yaendayo haraka (BRT), njia za juu makutano ya Tazara na Ubungo, barabara pete "Dar es Salaam Outer Ring Roads", barabara ya Dar es Salaam kwenda Chalinze "Express way", upanuzi wa barabara ya lami sehemu ya Gerezani pamoja na ujenzi wa daraja la Kigamboni.

Blogu hii inaomba mamlaka itakayokuwa inasimamia kivuko hiki kujitahidi kukitunza ili malengo yaliyokusudiwa yatimie. Pia Blogu hii inazidi kuiomba serikali pamoja na Wizara ya Ujenzi kununua kivuko kingine. Lengo la kununua kivuko kingine ni kuwa wakati kivuko kimoja kinatoka Bagamoyo basi kuwe na kingine kinachotoka Dar es Salaam kwa wakati huo huo ili wananchi wasisubiri kivuko kwa muda mrefu.

Picha: Michuzi Blog

Wednesday, October 22, 2014

Hongera Manispaa ya Temeke kwa ujenzi wa barabara inayoingia uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam

Hongera Manispaa ya Temeke kwa ujenzi wa barabara inayoingia uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Barabara hii fupi inaunganisha ofisi ya manispaa ya Temeke na barabara ya Taifa. Awali haikuwa barabara ya lami. Blogu hii inaomba manispaa hii kuzidi kutenga mafungu ya fedha ili kuziwekea lami barabara zinazozunguka uwanja huu muhimu wa taifa. Kuna mitaa karibu na manispaa ya Temeke ambayo nayo inahitaji kuwekewa lami ili sehemu hii muhimu ya kimataifa ipate hadhi inayostahili. Eneo hili ni muhimu licha ya kuwa na Makao Makuu ya Manispaa ya Temeke, na Uwanja wa Taifa, pia kuna chuo kikuu kishiriki cha Elimu, DUCE pamoja na uwanja wa UHURU ambapo ni sehemu ambayo Taifa hili lilipata uhuru wake miaka ya sitini.

Blogu hii inaiomba manispaa ya Temeke pia kuangalia uwezekano wa kujenga kituo kikuu cha mabasi ya abiria pamoja na "parking" kubwa ya magari kwa ajili ya mechi kubwa kubwa za mpira wa miguu. Hii licha ya kuwasaidia wananchi na hasa wapenzi wa kandanda pia itaongeza mapato kwa manispaa hii siku za usoni.

Barabara mpya ya lami iliyojengwa kuunganisha na barabara ya 
Taifa (Picha, tuijengetanzania.blogspot.com)

Mwonekano wa uwanja wa UHURU (bado matengenezo yana 
endelea ya uwanja huo) ambapo barabara mpya inaelekea uwanja 
huo pamoja na uwanja waTaifa (Picha, tuijengetanzania.blogspot.com)


Barabara mpya ya lami iliyojengwa kuunganisha na barabara ya 
Taifa (Picha, tuijengetanzania.blogspot.com)

Sunday, August 24, 2014

Hongera Rais Kikwete kwa kuahidi kuboresha sekta ya huduma ya afya kwa njia ya mtandao


Image result for kikwete
Picha: en.wikiquote.org     

Picha: ippmedia.com

Hongera Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa kuahidi kuboresha sekta ya huduma ya afya kwa njia ya mtandao.

Rais alisema hayo wakati akizungumza na wananchi wa vijiji vya Kisaki, Matombo, Dutumi na Kinole Morogoro vijijini. Aidha alisema huduma itakayotolewa itapunguza vifo vya wagonjwa hasa akina mama wajawazito na watoto.

Huduma ya matibabu kwa njia ya mtandao itafanya mawasiliano ya moja kwa moja kutoka kwa madaktari bingwa wa ndani na nje ya nchi wakati wa kutoa matibabu. Aidha, huduma ya mtandao imeonyesha mafanikio makubwa  kwa madaktari wa ngazi ya chini kuwasiliana na madaktari bingwa popote duniani na kuokoa maisha ya mgonjwa.

Blogu hii inaomba huduma hii itolewe nchi nzima hasa maeneo ya vijijini. Blogu hii inasisitiza kuwa kutokana na maendeleo ya teknolojia hasa ya simu na internet inawezekana huduma ya namna hii kutolewa bila tatizo lolote. 

Ni rahisi kutoa visingizio kuwa baadhi ya vijiji nchini havina umeme wa kuchajia simu na vifaa vya kielektroniki. Lakini huduma za solar, betri za magari makubwa, pamoja na booster charger za kisasa zinasaidia katika kupatikana kwa nishati. Suala linalotakiwa ni kwa Wizara ya Afya pamoja na halmashauri za miji na mikoa kujipanga katika kufanikisha huduma ya afya kwa njia ya mtandao ili kuokoa maisha ya watanzania hasa wakina mama na watoto. 

Tuesday, August 12, 2014

Hongera Serikali kwa kuahidi kujenga barabara 4 za juu ‘flyover’ jijini Dar es Salaam ndani ya kipindi cha miaka 3

Hongera Serikali ya Jamhuri wa Tanzania, kupitia Wizara ya Ujenzi kwa kuahidi kujenga barabara nne za juu ‘flyover’ jijini Dar es Salaam ndani ya miaka mitatu ijayo. Hayo yamesemwa na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli. Pia Mh Magufuli amesema Daraja la Kigamboni litakamilika ifikapo Juni mwakani.
Aidha Waziri wa Ujenzi amesema Serikali imetenga Sh2 bilioni kwa ajili ya kununua kivuko cha mwendo kasi kitakachokuwa kikitoa huduma kati ya Dar es Salaam na Bagamoyo pamoja na kukamilika kwa ujenzi wa barabara za pembezoni ndani ya jiji la Dar es Salaam.
Mh Magufuli amesema barabara za juu zitakazojengwa ni Tazara, Ubungo, Gerezani na DIT (Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam) na kuwaahidi watanzania kuwa ndani ya miaka mitatu foleni katika jiji la Dar es Salaam itakuwa historia.
 
Blogu hii inaipongeza Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi kwa kuwa na lengo hili zuri ambalo litapunguza foleni jijini Dar es Salaam. Kupungua kwa foleni jijini Dar es Salaam kutaleta manufaa kwa wakazi wa jiji hili pamoja na kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na jiji kwa ujumla. Aidha blogu hii inaomba juhudi hizi za Serikali ziende katika miji mingine mikubwa kama Arusha, Mwanza, Dodoma, Mbeya n.k.
 
Aidha, ombi la blogu hii ni kwamba Taifa lisisubiri kuwepo kwa foleni katika miji mikubwa ila ijiandae kabla idadi ya magari haijawa mengi. Kwa habari zaidi soma mwananchi.
 
Picha: mwananchi

Saturday, July 26, 2014

Hongera DUCE na Wizara ya Elimu kwa ujenzi wa Jengo la Mihadhara timilifu. Wengine waige

Jengo la mihadhara katika  Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu. Unaweza kuona jengo lina 
mihadhara mitatu tofauti, nje kuna vitofali na njia ya lami pamoja na bustani na miti. 
Huu ni ujenzi kamili "timilifu" (Picha: Geofrey Kalumuna) 

Jengo hilo ni ukumbi mkubwa wa mihadhara katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu, DUCE (Dar es Salaam University College of Education), kilichopo jijini Dar es Salaam. Jengo hili lina mihadhara mitatu (3) kwa ajili ya kutoa mihadhara kwa wanafunzi wanaochukua shahada ya kwanza na diploma ya juu ya elimu. Mhadhara mmoja unaweza kuchukuwa wanafunzi na watu wengine waliokaa elfu 1 (1,000) kwa wakati mmoja.

Aidha jengo hili hutumika katika kuendesha mikutano mikubwa ya chuo, wanachuo pamoja na wadau wengine kutoka nje ya chuo kwa ruksa maalum. Blogu hii imeona itoe habari hii ili vyuo vingine nchini Tanzania viige mfano huu mzuri wa kuwa na zaidi ya mihadhara mitatu katika jengo moja ambapo shughuli tatu tofauti kwa watu wengi zinaweza kufanywa bila bughuza yoyote. 

Ndani ya jengo hili kuna huduma mbalimbali za ki-Tehama kwa ajili ya kurahisisha mihadhara. 

Kilicho ifurahisha zaidi blogu hii ni ujenzi "timilifu" unaojali mazingira, nje ya jengo kuna bustani nzuri, vitofali vinavyozuia vumbi na tope, pia pembeni kuna viti na meza za tofali nzuri kwa ajili ya watu kupunzika na wanafunzi kujisomea (vimbweta). Blogu hii kwa kutumia mfano huu wa DUCE, kuwa ni vyema kama kuna majengo ama barabara zinajengwa basi zijengwe "kikamilifu" ili kujali watu wote. Mfano kama tunajenga majengo tuzingatie pia mazingira nje ya jengo ama barabara. Ni vyema kama barabara inajegwa kuwe na njia kwa ajili ya watu, baiskeli na walemavu ambazo zina vitofali ili kuepuka vumbi wakati wa kiangazi ama tope wakati wa mvua. 

"Kwa maneno mengine haifurahishi kujenga jengo zuri lakini nje kuna tope ama vumbi ama kujenga barabara nzuri ambapo watu wanapita pembeni kwenye vumbi ama tope. Watanzania kwa hili tunaweza"

Hongera DUCE na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa kujenga jengo la namna hii. Hongera pia kwa ujenzi timilifu. Kasi hii iendelezwe kwa vyuo vingine nchini ili vijana na watoto wetu wapate sehemu ya kupata mafunzo ya elimu ya juu kwa ubora unaostahili.

Saturday, July 19, 2014

Hongera TFF kwa kuanza kuuza tiketi za mechi za soka kwa njia ya kieletroniki kati ya Taifa Stars na Timu ya Taifa ya Msumbiji

Hongera Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) kwa kuanza kuuza tiketi za mechi za soka kwa njia ya kieletroniki. Hakika blogu hii imefurahishwa sana na hatua hii ya maendeleo katika soka la Tanzania. Hivi karibuni TFF imetangaza kuuza tiketi za mchezo kati ya Timu ya Taifa ya Tanzania "Taifa stars" na Timu ya Taifa ya Msumbiji "Mambas" utakaofanyika jumapili 20 Julai 2014. 

Utaratibu huu licha ya kuboresha mapato yatokanayo na uuzaji tiketi nchini pia unawawezesha wapenzi wa soka kununua tiketi bila taabu. Ni simu yako ya mkononi ndiyo itakuwezesha kununua tiketi yako. 

Blogu hii inaomba utaratibu huu uwe wa kudumu na hasa kwa mechi za ligi kuu ya Tanzania Bara. Hongera sana TFF, Jamal Malinzi (Rais wa TFF), wajumbe wa kamati ya utendaji ya TFF, watendaji na wafanyakazi wa TFF, Max-Malipo na M-Pesa. Hakika maendeleo ya soka Tanzania yanawezekana!!

Ili kupata tiketi yako tumia M-PESA kwa kupiga *150*00# Kisha Bonyeza 4, Bonyeza tena 4 kisha weka Namba ya Kampuni 173399 Kisha Ingiza 7000 kama Namba ya Kumbukumbu ya Malipo, kisha andika tena 7000 kwenye Weka kiasi, Kisha weka namba ya siri na Baadaye bonyeza  1 Kukubali. Hapo utapokea ujumbe wenye orodha ya vituo vya MaxMalipo vya kuchukua tiketi ukiwa na namba ya uhakiki wa malipo yako.

Picha:tffnews.blogspot.com

Monday, July 7, 2014

Hongera VETA kwa kupata TUZO kwenye maonyesho ya 77 katika kipengele cha utoaji mafunzo na ujuzi

Hongera MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa kupata TUZO kwenye maonyesho ya Sabasaba katika kipengele cha kundi la utoaji mafunzo pamoja na ujuzi nchini.
Hakika blogu hii imefurahishwa na juhudi za VETA katika kuwapa wananchi hasa vijana ujuzi ili kukabiliana na changamoto zilizopo nchini. Ujuzi wanaoupata vijana unawasaidia kuinua uchumi wa mtu moja moja na taifa kwa ujumla.
Blogu hii inaomba VETA izidi kutoa mafunzo mbalimbali kwa vijana na hasa walio katika mikoa na wilaya za pembezoni ili faida ya mafunzo iwe kwa taifa zima. Pia blogu hii inawaomba vijana bila ya kujali elimu walionayo kwa sasa kujiunga na vyuo vya VETA ili kupata ujuzi na maarifa ya kutenda kazi kivitendo. Nchi nyingi zilizoendelea na zinazoendelea zimetilia mkazo mafunzo ya namna hii "Vocational and Technical Education". Uwepo wa mafunzo ya namna hii huziwezesha nchi zilizoendelea na zinazoendelea kupata Nguvu Kazi yenye ujuzi na maarifa katika nyanja mbalimbali kama vile ufundi mchundo, ufundi makenika, ufundi uashi, ufundi bomba, watengeza vywele, wapaka rangi, mafundi wa kompyuta na magari, madereva wa magari makubwa kama matreka, maroli, waendesha mitambo na mashine kubwa, wahudumu wa hoteli, waongoza watalii nk.
Maendeleo ya taifa lolote yanakuwa shakani bila ya kuwa na watu wa namna hii katika nchi ambao wamepata mafunzo rasmi ya ufundi stadi katika nyanja mbalimbali.Mfano, huwezi jenga barabara zenye uhakika bila ya kuwa na watu waliopitia VETA katika fani ya ujenzi. Nchi yetu ina mafundi wengi sana ambao hawajapitia VETA, na hivyo ubora wa huduma zao kuwa hafifu. Pia taifa linapaswa kupitisha sheria kwa kazi za namna hii zifanywe na wale tu walioudhuria mafunzo ya namna hii na kufaulu. Unataka kujiunga na VETA? Bonyeza hapa.
Picha: veta.go.tz